Twitter

Twitter Buttons

Wednesday 14 August 2013

Vipaumbele Vya Michezo Vizingatie Ufanisi


Nchi za ukanda wa Afrika Mashariki ziko nyuma sana katika michezo, pengine kuliko ukanda mwingine wowote hapa Afrika.
Ukilinganisha na majirani nchi jirani, hali ni mbaya zaidi kwa Tanzania. Hili utaligundua kwenye mashindano ya ndani ambayo hayahusishi timu za taifa, mfano mashindano ya vyuo vikuu na shule za sekondari. 

Miaka yote tumekuwa tukilalamikia maandalizi duni na visingizio vya kufanana na hivyo lakini ukitazama jinsi nchi kama Kenya na Uganda zinavyotia mkazo michezo mashuleni ni wazi kuwa tunastahili matokeo tunayoyapata.

Mara kadhaa nguvu za serikali na wadau zimekuwa katika timu chache za taifa, hasa soka na kuitenga michezo mingine. Hata bajeti ya Wizara husika hujikuta ikitumika sana kuhudumia soka kuliko michezo mingine.
Pamoja na ukweli kuwa kuboresha michezo kunahitaji fedha na mipango ya muda mrefu, kuna baadhi ya nchi zina nafasi ya kufanya vizuri kuliko zingine kutokana na sababu za kimazingira.

Tunaweza kujiuliza kwanini Kenya na Ethiopia hufanya vizuri kwenye mbio ndefu kuliko mataifa mengine?  Si kwamba Kenya wamewekeza sana kwenye riadha kuliko mataifa ya Ulaya, lakini mahali walipo na aina ya watu walionao kunawawezesha kufanya hivi.
Inaweza kuchukuliwa kama mtazamo wa kikabila, lakini ukweli ni kuwa wanariadha wanaofanya vizuri kutoka Kenya huwa ni wa makabila fulani tu, hasa jamii za Kifugaji za Nandi, Kalenjen na Maasai. 

Isaiah Kiplagat, Peter Cheruiyot, Pamela Jelimo, Vivian Cheruiyot na Prisca Cherono ni miongoni mwa wanariadha mahiri ambao wanatoka katika jamii za wafugaji.
Utafiti uliofanywa na Scott na wenzake miaka ya 2005 na 2009 nchini Ethiopia na Kenya ulibaini kuwa watu wa jamii za eneo la Arsi, Ethipia na Mlima Kenya wana vinasaba ambavyo vinawawezesha kuwa wakimbiaji mahiri wa mbio ndefu. Inashangaza kuona eneo ambalo wakazi wake hawafiki asilimia 0.1 ya wakazi wa dunia kuwa na medali zaidi ya 50 za michezo ya Olimpiki.

Tafiti fulani za mwaka 2007 huko Kenya zilidai  kuwa jamii za Kifugaji hutoa wakimbiaji mahiri kutokana na matumizi makubwa ya maziwa ya ng’ombe.
Majibu tafiti hizi yanaweza yasiwe sahihi kwa asilimia zote lakini hata ukitazama nchini kwetu, wakimbiaji mahiri walioipa sifa nchi hii kama Filbert Bayi, Francis Naali na Wilhelm Gidabuday wanatoka kwenye jamii hizi hizi za kifugaji.
Kukimbia riadha kwa vijana wadogo wa jamii za hizi za Kaskazini, sio tu mchezo wa mashindano, lakini pia ni hulka na mchezo wa kujifurahisha, kama vile soka ilivy katika jamii nyingi.

Laiti kama Chama cha Riadha (AT) kingeelekeza nguvu nyingi katika kuboresha mazingira ya riadha kwa chipukizi wa jamii za wafugaji pengine tungekuwa na medali nyingi zaidi za riadha katika mashindano kama vile IAAF, Diamond League,  Olimpiki na mengineyo.

Mchezo wa kuogelea ni moja ya michezo ambayo tunaweza kunufaika  nayo. Hapa tulipo tayari tuna waogeleaji ambao hawakupita shule yoyote ya michezo lakini tayari ni mahiri. Wengi  wao hutoka visiwani kama vile Zanzibar, Ukerewe, Mafia na sehemu za pwani kama Dar es Salaam na kadhalika.
Kama ukibahatika kutembelea ufukwe wa Coco siku za wikiendi, wapo vijana ambao hucheza mchezo wa kujirusha kwenye maji kwa kujifurahisha tu. Kama mtu anaweza kucheza mchezo kwa kujifurahisha, kwanini asitengenezewe mazingira mchezo huo ukampa faida?

Mara nyingi tumehangaika kuwapa hamasa wachezaji wetu wanapocheza mashindano ya kimataifa, hatuoni kwamba tukiwa na wachezaji wa aina hii tayari ni hamasa tosha?
Pengine Chama cha Kuogelea (kama kipo) hakijafanya tafiti kujua wapi hasa tuweke msisitizo katika kukuza vipaji vya waogeleaji. Si kila shule inaweza kufundisha kuogelea na kukawa na mafanikio. Mahali ambapo maji ya kunywa hufuatwa kilomita tano huwezi kupata waogeleaji kwa namna yoyote.

Mbio za baiskeli ni mchezo mwingine ambao tunaweza kufanya vizuri kama tutaamua kuchanga karata zetu vizuri. Wakazi wa kanda ya ziwa ni waendeshaji mahiri wa baiskeli na hata vijana wamejiajiri katika sekta ya usafirishaji kwa kutumia njia ya baiskeli.
Mara kadhaa tumeshuhudia mikoa ya Mwanza na Shinyanga wakiwa wenyeji wa mbio za Baiskeli lakini sina hakika kama tulishawahi kufikiria kuiwakilisha nchi katika mashindano ya kidunia kama Tour de France.
Kwa jicho jepesi, naona tunao uwezo wa kushiriki mashindano haya bila kikwazo chochote. Wasafirishaji wa abiria kwa njia ya baiskeli huweza kumbeba mtu mwenye uzito wa kilo 70 au 80 kwa umbali wa kilomita kadhaa. Ni wazimu kudhani kuwa hawataweza kushindana na waendeshaji wa kimataifa ambao hutumia baiskeli nyepesi zisizo na mzigo wowote.
Hapa tunahitaji mafunzo machache tu ya kuwawezesha vijana hawa kuendesha baiskeli kwa viwango vya kimataifa na miaka kadhaa mbele tutakuwa na wawakilishi katika Tour de France.

Michezo ni ajira na sehemu ya kukuza uchumi, kama nafasi ipo ya kufanya vijana wetu wanufaike na michezo wanayoiweza tufungue macho. Tusiishie kufundisha michezo ile ile kwenye mitalaa yetu miaka nenda rudi. Vipaumbele vya vyama vya michezo na Baraza la Michezo vizingatie ufanisi wa maeneo husika katika michezo wanayoisimamia.
Nchi kadhaa duniani zimeshajipambanua na kuweka nguvu zao katika michezo wanayoiweza hata kama haina mashabiki wa kutosha kama ilivyo mingine. Ni wakati wa sisi kutazama kipi tunakiweza zaidi na tuwekeze huko kwa nguvu zote.

Mwandishi:  Mphamvu Daniel
Simu; 0717474832
Barua pepe; mphamvu@facebook.com

No comments:

Post a Comment