Twitter

Twitter Buttons

Friday 23 August 2013

Ligi Kuu 2013/2014; Ndoto za Ubingwa Azam, Na Kamari ya Stewart Hall

                              


Licha ya uwekezaji wa kiwango kikubwa , ubingwa wa ligi kuu umeendelea kuwa simulizi ya ‘msimu ujao’ kwa vijana wa Chamazi. Kwa misimu miwili mfululizo, wamekaribia sana kutwaa ubingwa lakini mara zote wamefia ufuoni na kuwaacha wakongwe Simba na Yanga wakishangilia. Kwenye msimu huu mpya, Kwa mara nyingine watajitupa kwenye ulingo kupigania ubingwa wa ligi kuu. Licha ya kushiriki michuano ya Afrika, akili na nguvu zao zitakuwa zimeelekezwakwenye ligi kuu kuhakikisha wanapambana mpaka dakika ya mwisho kuchukua ubingwa. Ndio kombe la msingi zaidi  kwao licha ya kuwa kombe la shirikisho ni kubwa zaidi. Kombe la shirikisho litabaki kuwa mazoezi ya ndoto zao za siku za usoni.

Azam,licha ya kuhesabika kama moja ya vigogo vya soka nchini, bado hawajaingia rasmi katika historia ya vigogo wa soka nchini. Ubavu wao wa fedha unaweza kuwa umewapa heshima ya kuitwa vigogo lakini kihistoria wao bado ni kinda kwa Coastal Union, Mtibwa Sugar na Pamba . Hivi ni baadhi tu ya vilabu ambavyo vipo katika kumbukumbu za historia za ubingwa Tanzania. Kwa sasa Azam ni vigogo lakini ni kofia ya ubingwa tu ndio itawapa heshima na hadhi ya kuitwa vigogo wa soka nchini. Jeuri ya pesa inaipa klabu ukuu wa muda tu, ubingwa unatoa hadhi ya kihistoria. Mwisho wa siku, historia huandikwa na mabingwa tu. 

Azam waliingia kambini mapema, wamefanya ziara ya siku kumi huko Afrika Kusini Pamoja na mikakati mingine katika jitihada zao za kujifua kwa ajili ya mbio za ubingwa wa ligi kuu. Licha ya yote hayo,kamari kubwa zaidi waliyocheza ni kutosajili wachezaji wapya kwa msimu huu. Ni ngumu kuamini kuwa  ni mkakati wa utawala kuamua kutosajili hasa baada ya kukaribia sana kutwaa ubingwa msimu uliopita. Kwa namna yoyote ile utakuwa ni uamuzi wa kocha wao. 

Inawezekana kocha Stewart Hall ameamua kutengeneza mshikamano na umoja katika kikosi kuliko kusajili wachezaji wapya ambao watachukua muda kuelewana. Ameamua kuwafyeka baadhi ya wachezaji ambao ameona hatawahitaji na kupandisha chipukizi kadhaa. Kati ya waliokumbwa na panga ni Pamoja na kiungo mshambuliaji, Abdi Kassim, Abdulhalim Humud na kipa Munishi. Jambo la kustaajibisha ni kuwa wawili kati ya watatu waliotemwa,Munishi na Humud wameibukia kwa wapinzani wao wakubwa, Simba na Yanga. Kama filamu ya kejeli hivi, Munishi katika mechi yake ya kwanza aliizuia Azam kuchukua ubingwa wa kombe la ngao ya jamii kwa kuokoa hatari zote zilizoelekezwa langoni mwake.

Humud, kiungo matata, ambaye kama akitulia na kuamua kucheza mpira Azam wanaweza kujikuta wakimwaga machozi kwa kuwapa silaha wapinzani wao. Kwenye biashara za kuwania ubingwa ni kosa kubwa kumpa unafuu adui yako lakini Azam ni kama wamefanya hivyo kwa kuwaimarisha Simba na Yanga. Suala la kutemwa kwa Abdi Kassim lina utata zaidi hasa baada ya kila upande kutoa kauli tofauti. Kwa waliofuatilia ligi msimu uliopita watagundua kuwa licha ya kuonekana kuwa umri umemtupa mkono bado Babbi alitoa mchango mkubwa wa magoli.

Bila ya Abdi Kassim na huku Humphrey Mieno akiwa majeruhi, Azam wanaweza kujikuta wakiwa hawana kiungo mshambuliaji wa kuwasidia ufungaji. Ukichungulia kwa wapinzani wao, Simba na Yanga utagundua wako vyema kwa kuwa na Amri Kiemba na Haruna Niyonzima. Kuna wakati washambuliaji wa Yanga walikuwa likizo ya kufunga lakini Niyonzima na Nizar Khalfan wakabeba majukumu vizuri .Yanga ilijikuta ikiambulia ushindi wa bao moja mfululizo kutokana na viungo washambuliaji kuwasaidia washambuliaji na hivyo kujikuta timu ikisonga mbele bila kuyumba. Kwa upande wa Simba, mchango wa mabao wa Amri Kiemba unajulikana.Kwa misimu miwili mfululizo sasa, Kiemba amekuwa msaada mkubwa kwa Simba kutokana mabao anayofunga. Kwa jicho la haraka, utagundua Azam hawana mtu wa hivyo msimu huu. Wamemtema Abdi Kassim na kushindwa kuziba pengo lake.

Ni jambo la kusubiri na kuona mwisho wa msimu utakuaje licha ya kuwa kuna dirisha dogo la usajili baada ya mzunguko wa kwanza. Stewart anaweza kusajili kipindi hicho lakini kama watakuwa wamevurunda na kuachwa na Simba au Yanga basi itabidi wasahau ubingwa kwa mara nyingine.Simba na Yanga wakikutanguliza ni ngumu sana kuwakamata kwa kuwa mashabiki wao wanakuwa nyuma yao kuwahamasisha. Kwa kucheza kamari ya kutosajili Stewart Hall anaweza kuibuka shujaa au kuishia kufungasha virago na kurudi katika fukwe baridi za vya Uingereza.

No comments:

Post a Comment