Twitter

Twitter Buttons

Monday 26 August 2013

Jicho Kwa Mafahali Watatu: Yanga Mteremko...Simba na Azam Hesabu.


                                  
Msimu wa 2013/2014 wa ligi kuu ya Vodacom ndio umeanza rasmi kwa mechi za raundi ya kwanza kuchezwa mwisho wa juma. Mechi za kwanza zimeshuhudia mabingwa watetezi , Yanga wakiibuka na ushindi mkubwa zaidi. Chini ya kocha wao Mholanzi Ernie Brandts waliiporomoshea kipigo cha mbwa mwizi timu ya Ashanti United iliyopanda daraja msimu huu.

Yanga ilitarajiwa kushinda lakini si kwa kutoa kipigo cha 5-1, hili halikutarajiwa na wengi hasa ukizingatia kuwa Ashanti walionekana kuwa wamejikakamua kwa maandalizi ya kutosha. Ashanti walipiga hatua hadi ya kufanya ziara nje ya nchi katika kujiandaa na ligi. Wengi tulitarajia kuwa watatoa ushindani kwa Yanga. Kinyume na matarajio wameambulia kipigo ambacho kinaweza kuwa kipigo kikali zaidi katika msimu mzima.

Ingawa  msimu ndio umeanza, lakini Yanga wanaonekana kuwa kamili sana ukilinganisha na wapinzani wao. Ukamili wa Yanga hautokani na kuwa na wachezaji bora kulinganisha na Simba na Azam, la hasha, wapo bora kutokana na mbinu za kocha wao. Kwa mchezaji mmoja mmoja, Simba na Azam wanaweza kuwa bora kuliko Yanga na pia wanaweza kuendelea kutoa wachezaji wengi katika timu za taifa. Japo ni mapema sana lakini tunaweza kushuhudia filamu ya msimu uliopita ya wachezaji wa Simba na Azam kutamba katika timu ya taifa huku Yanga wakitesa kwenye mbio za ubingwa. 

Ubora wa Yanga unatokana na mbinu za kocha wao kucheza mchezo wa kushambulia moja kwa moja. Wako ‘direct’, wanatumia pasi chache kulifikia lango la adui kulinganisha na wapinzani wao, Azam na Simba. Yanga wana wachezaji wengi wenye kasi, kuanzia Msuva, Juma Abdul, Salum Telela hadi ingizo jipya Mrisho Ngassa. Hawa ni hatari hasa wakikuta walinzi waliozubaa. Ni tofauti na Azam na Simba ambao wanapendelea zaidi kumiliki mpira hasa kwenye maeneo yasiyo na madhara kwa adui.

Ikumbukwe kuwa kocha Ernie Brandts alikuta ligi ya msimu uliopita imekwishaaanza licha ya kuwa aliweza kubeba ubingwa. Msimu huu Yanga inaweza kuwa hatari zaidi kwa kuwa kocha ameanza na timu toka mwanzo na hivyo kupata muda mwafaka wa kushughulikia mapungufu.
Jambo la hatari zaidi kwa wapinzani  wenye ndoto za kuwapokonya ubingwa Yanga ni jeshi la mashabiki lililo nyuma ya Yanga hasa kwa kasi walioanza nayo. Hakuna shaka kuwa Yanga inaongoza kuvutia mashabiki uwanjani na hasa timu yao inapokuwa katika wimbi la ushindi basi mashabiki wake huongezeka maradufu.

Azam anaanzia ugenini mechi tatu za kwanza,ni ratiba ngumu kwake. Ameanza kwa sare na Mtibwa Sugar kisha anamfuata Rhino Rangers kabla ya kumalizana na Kagera Sugar huko Kaitaba. Simba naye anaanzia ugenini mechi mbili za kwanza, ameanza kwa sare dhidi ya Rhino kasha anawafuata wanajeshi wengine, JKT Oljoro kabla ya kupambana na Mtibwa Sugar nyumbani. Kwa haraka haraka utaona kuna hatari ya Azam na Simba kujikuta wakiwa nyuma ya Yanga kwa pointi kadhaa ndani ya raundi tatu tu za mwanzo. Yanga wao wanaanzia nyumbani mechi mbili za kwanza,wamemsarambatuisha Ashanti, Coastal anawafuata kabla ya wao kusafiri kwa kuku mgeni wa ligi, Mbeya City.

Simba na Azam itawabidi kuchanga karata zao vizuri ili wasije kujikuta wanatimuliwa vumbi  baada ya raundi chache tu za mwanzoni. Yanga wakitoka, wapinzani wahesabu maumivu. Ni hatari kuwaacha Yanga watangulie mbele, hasa Yanga hii chini ya mholanzi.

No comments:

Post a Comment