Twitter

Twitter Buttons

Thursday 4 April 2013

Gor Mahia Ndani Ya Kinywa Cha Mamba



                               
       GOR  MAHIA NDANI YA KINYWA CHA MAMBA
Macho na masikio ya wapenda kandanda nchini Kenya yataelekezwa kwenye dimba la Nyayo mwishoni mwa juma hili. Pambano litakalovuta hisia zote ni baina ya miamba wa Kenya, Gor Mahia itakayoluwa na kibarua kigumu dhidi ya wajukuu wa Farao,ENPPI ya Misri. Gor Mahia ina kibarua cha kulipa kisasi cha mabao 3-0 ili kuweza kupata nafasi ya kusonga mbele kwenye kombe la shirikisho  Afrika ngazi ya vilabu.

Kila masaa yanavyokatika ndivyo homa ya mpambano huu inavyozidi kupanda hasa kwa maelfu ya wapenzi na wanazi wa Gor Mahia. Kinachotia shaka si uwezo wa Gor Mahia bali ni ukubwa wa kipigo chenyewe.Ni dhahiri kuwa  kwa kuruhusu mabao matatu kule Misri Gor Mahia ni kama walikubali kuingia kwenye mdomo wa mamba. Mabao matatu ni mengi mno  kwa timu yoyote ile. Kazi iliyopo mbele si haba,inahitaji  mioyo ya chuma na roho za sabuni kukabiliana nayo.

Hata hivyo waswahili hunena mbwa hafi aonapo ufuo hasa ikizangatiwa kuwa Gor Mahia watacheza mbele ya maelfu ya jeshi lao la mashabiki watakaokuwa wakishangilia kwa mbwembwe zote. Itawabidi mashabiki wa Gor Mahia kupasuka koo kwa kupaza sauti kuishangilia timu yao toka kipenga cha kwanza hadi cha mwisho . Mashabiki watakuwa kama mchezaji wa kumi na  mbili uwanjani katika kuhakikisha ushindi unapatikana.

Licha ya kuwa Gor Mahia bado haijashika ule moto wake wa msimu uliopita bado kuna matumaini makubwa hasa ukiangalia aina ya wachezaji walio nao kikosini. Licha ya mkufunzi wao, Logarusic,  kulililia kuwa majeruhi yamewaathiri sana bado ana silaha zinazoweza kuiangamiza ENPPI kama akizumia ipasavyo.

Taratibu mshambuliaji hatari,Dan Sserenkuma anaanza kurudisha makali yake  ya msimu uliopita. Pia mshambuliaji chipukizi aliyesajiliwa msimu huu kutoka KCB, Paul Kiongera anazidi kuimarika kwa kuwaonesha mashabiki  thamani yake. Ikumbukwe Kiongera alianza kwa kusuasua kiasi cha kuzomewa na baadhi ya mashabiki kwenyi mechi za awali. Wasi wasi unabakia kwa pacha wa Sserenkuma,Rama Salim ambaye bado anaweweseka. Ushirikiano wa Rama Salim na Dan Sserenkuma ulikuwa chachu kuu ya mafanikio ya Gor Mahia mwaka jana.

Safu ya ulinzi si mbaya,golini Jerim Onyango au Ivo Mapunda wote wapo kamili,Donald Mosoti,David Owino aliyezima moto wa Victor Moses wa Chelsea katika mechi dhidi ya Naijeria,Ivan Anguyo licha ya kuwa ameonesha udhaifu pamoja na Wekesa wana uwezo wa  kuzima mashambulizi ya ENPPI.Kazi yao itakuwa kuhakikisha  ENPPI  hawapati bao lolote  linaloweza kuharibu hesabu za Gor Mahia.
Safu ya Kiungo itakuwa na kazi ya kupika nafasi za mabao kwa washambuliaji huku pia wakiipa kinga safu ya ulinzi dhidi ya mashambulizi ya ENPPI.Bila shaka,Teddy Akumu,Ali Abondo,Njuguna na Kevin Abondo  wataweza kuwapa raha mashabiki wa Gor Mahia na kuhakikisha klabu ya Kenya inaonja ladha ya ushindi dhidi ya wamisri.
SOFAPAKA waliweza kuitoa Ismailia licha ya kufungwa 3-0 ugenini , ni jambo ambalo Gor Mahia pia wanaweza kulifanya.Uwezo wanao, sababu za kufanya hivyo wanazo, na pia nia ya kufanikisha jambo hilo wanayo.Kila la kheri Gor Mahia katika jitihada zenu za kujitoa kwenye kinywa cha mambo.

No comments:

Post a Comment